
Kigali, Rwanda
Serikali ya Rwanda imesema ndege ya kivita kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo ilikiuka mamlaka ya anga yake Jumanne, wakati mzozo ukizidi kati ya majirani hao kuhusiana na eneo tete la mashariki ya Congo.
Kinshasa ilikanusha kuwa moja ya ndege zake iliruka juu ya Rwanda, na kuishutumu Kigali kwa “mashambulio” dhidi ya ndege ambapo ilisema ni “kitendo cha vita”.
Uhusiano tayari umezorota kati ya majirani hao, huku DRC ikiishutumu Rwanda kwa kuunga mkono kundi la waasi la M23, ambalo limeteka maeneo mengi ya ardhi ya Congo miezi ya hivi karibuni.
Kigali inakanusha madai hayo yanayoungwa mkono na wataalamu wa Umoja wa Mataifa, Marekani, Ufaransa na Ubelgiji.
Kwa upande wake, Rwanda inaishutumu Kinshasa kwa kushirikiana na FDLR-kundi la zamani la waasi wa Kihutu wa Rwanda lenye ngome yake DRC.
“Ndege ya kivita chapa ya Sukhoi-25 kutoka DR Congo imeingia anga ya Rwanda kwa mara ya tatu,” juu ya wilaya ya Rubavu, karibu na Goma,” msemaji wa serikali ya Rwanda Yolande Makolo alisema katika taarifa.
“Hatua za ulinzi zimechukuliwa,” alisema, na kuongeza: “Rwanda inaiomba DRC kukomesha uchokozi huu.”
Visa viwili vya mwisho viliripotiwa mwezi Novemba na Desemba na vilifuatiwa na maandamano mjini Kigali.
Waandishi wa habari wa AFP mjini Goma, mashariki mwa DRC walisikia mlipuko mkubwa uliofuatiwa na milio miwili ya risasi wakati ndege ya Congo ikiruka Jumanne mchana.
Video iliyowekwa kwenye mitandao ya kijamii ilionesha mwako karibu na mpiganaji huyo, ambayo ilitua kwenye uwanja wa ndege wa Goma.
Taarifa ya serikali ya DRC ilisema ndege hiyo ya kivita “ilishambuliwa ilipokuwa ikitua katika uwanja wa ndege wa Goma.”
“Risasi za Rwanda zilielekezwa dhidi ya ndege ya Congo iliyokuwa ikiruka ndani ya ardhi ya Congo. Haikuruka juu ya anga ya Rwanda. Ndege hiyo ilitua bila uharibifu mkubwa,” iliongeza taarifa hiyo.
‘Kitendo cha uchokozi wa maksudi’
Kinshasa ilisema inachukulia tukio hilo kuwa “kitendo cha uchokozi wa makusudi” kinacholenga kuhujumu juhudi za amani mashariki mwa nchi. Taarifa hiyo ilisema serikali “inabakisha haki halali ya kutetea eneo lake la kitaifa.”
Mapigano kati ya wanajeshi wa Congo na M23, wanaopiga hatua kuelekea Goma, mji mkuu wa jimbo la Kivu Kaskazini, yamesababisha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kupeleka kikosi cha pamoja cha kikanda ili kukomesha ghasia hizo.
Chanzo: AFPE
Tarehe: 26.01.2023
Saa: 9 alasiri.
Tutumie maoni yako